KARIBU USOME HADITHI NZURI ZA KUSISIMUA

Chombezo : Mwajuma Utamu Sehemu Ya Mwisho


Nilichokisikia wakati nilipokuwa nimefumba macho yangu ni milio ya risasi, niliamini risasi hizo nilipigwa mimi, nilipoyafungua macho yangu kwa mara nyingine sikutaka kuamini kile nilichokuwa nikikishuhudia. Niliuona mwili wa Damian ukiwa chini huku ukitapatapa, damu zilikuwa zikimtoka kutokana na risasi alizokuwa amepigwa.

Ghafla! niliwaona polisi wakiwa ndani ya chumba hicho, sikutaka kuamini kile kilichokuwa kimetokea katika maisha yangu, yaani kama sio kutokea polisi ningeshakuwa maiti siku nyingi.
Polisi walinisaidia kunifungua kamba nilizokuwa nimefungwa nazo miguuni na mikononi, siku hiyo ndiyo ilikuwa mwanzo wa kuokoka na kifo nilichokuwa nimekikaribia.

Polisi walionekana kufanikiwa kazi yao kwa asilimia mia moja kwani muuaji huyo aliwasumbua mno, siku hiyo ndiyo walifanikiwa kumkamata na baada ya kumpiga risasi alifariki dunia hapohapo.
****
Baada ya kunisurika kifo na Damian au jini mweusi kama alivyokuwa akijulikana niliachana na biashara ya uchangudoa, sio mimi tu bali hata Suzie na yeye alichana na biashara hiyo.
Jambo la kushangaza baada ya Martin kurudi kutoka Dubai, Suzie aliitumia nafasi hiyo kumueleza kila kitu ambacho kilitokea katika maisha yangu.
Martin alinichukia baada ya kuambiwa hayo na kama haitoshi aliamua kuhamisha mapenzi kwa Suzie ambapo walifanikiwa kufunga ndoa na kubahatika kuzaa watoto mapacha, Gracious na Precious.
Niliumia sana baada ya tukio hilo kutokea hata hivyo sikuwa na wa kumlaumu, maisha yangu niliyachezea mwenyewe.
Baada ya kupita miezi mitatu niliamua kwenda kupima, majibu yalionyesha kuwa nilipata maambukizi ya virusi vya ukimwi hivyo nilitakiwa kuanza kutumia vidonge vya ARV kwa ajili ya kuongeza siku za kuishi.
Ni pigo kubwa katika maisha yangu, kiukweli najutia mambo mengi tena machafu niliyoyafanya katika maisha yangu, idadi ya wanaume niliyotembea nao inafika mia tatu.
Maisha ya mjini yalinishinda, niliuza kila kitu nilichoachiwa na Martin kama zawadi katika maisha yangu. Japokuwa ni miaka mingi sana imepita tangu nilipoondoka nyumbani kwetu Mtwara lakini niliamua kurudi.
Sikuwa ni Mwajuma yule wa zamani tena ambaye nilionekana kuwa mrembo wa sura mpaka umbo la kumvutia mwanaume yoyoye rijali, huyu wa sasa nilikuwa naishi na virusi vya ukimwi na muda wowote Mungu anaweza kunichukua kwani afya yangu imezidi kudhoofika.

FUNZO: Katika maisha wakati mwingine jifunze kutokana na makosa ya mtu mwingine, nimeamua kukusimulia kumbukumbu za maisha yangu ili na wewe ujifunze kutokana na makosa niliyoyafanya.
Naomba ukimaliza kuisoma kumbukumbu hii uyachukue yale yote mazuri kisha uyafanyie kazi na yale yote mabaya tafadhali naomba usiyachukue. Narudia tena katika maisha wakati mwingine jifunze kutokana na makosa aliyoyafanya mtu mwingine.

MWISHO.


Powered by Blogger.