KARIBU USOME HADITHI NZURI ZA KUSISIMUA

Simulizi : Singidani Sehemu Ya Nane (8)

Simulizi ya singidani
USO wa mzee huyu ulionyesha dhahiri kuwa hauna masihara; alitaka kujua jambo moja tu tena lenye hakika kutoka kwa mwanaye. Alitaka kujua kuhusu ndoa. Chris alitulia akimwangalia baba yake, kichwani akitafakari ni jibu gani lingemfaa baba yake.

“Chris niambie ukweli, umefikia wapi?” baba yake akamwuliza.

“Baba nilishakuambia kuwa lazima nitaoa mwaka huu kwa sababu tayari nimeshapata mchumba.”

“Sasa mbona unachelewesha mambo?”

“Si kuchelewesha baba, ni suala la mipango tu. Nipe muda.”

“Muda gani?”

“Miezi miwili inatosha kabisa, nipatie muda huo baba nitakamilisha hili suala.”

“Nataka iwe hivyo.”

Mzee Shila, baada ya kuzungumza hayo, alitoka haraka na kuelekea chumbani kwake, sebuleni alibaki Chris na mama yake tu. Waliangaliana kwa muda, kisha kila mmoja akajikuta akiinamisha uso wake chini.

“Lakini mwanangu, kwa nini usioe ili kuachana na haya manenomaneno ya baba yako?”

“Mama kwani nimekataa kuoa? Si tayari nimeshasema nimepata mchumba mama, kikubwa hapo ni muda tu.”

“Sawa.”

“Mama ngoja mimi niondoke, nina ratiba nyingi sana kesho asubuhi. Acha tu niende sasa,” akasema Chris akimtulizia macho mama yake.

“Sawa baba, usiku mwema.”

“Nanyi pia.”

***

Kichwa kilitaka kupasuka. Alitulia kitandani mwake akiwaza sana, dalili za kumpoteza mrembo Laura zilianza kuonekana waziwazi. Alitamani sana kumuoa Laura, hakuwa mwanamke wa kucheza naye kwa usiku mmoja tu!

Laura alikuwa mke!

“Lakini itawezekanaje wakati mzee naye analazimisha mke atokee kijijini?” akawaza Chris.

“Kuna kitu natakiwa kufanya hapa, lazima nimpate Laura maishani mwangu, siwezi kukubali akaolewa na mwanaume mwingine, haitawezekana hata kidogo,” akazidi kuwaza Chris.

Akiwa mawazoni, simu yake iliita. Haraka akaichukua na kuangalia kwenye kioo; akakutana na jina la Laura lilitokea. Akapokea haraka sana...

“Haloo mpenzi wangu...” sauti tulivu ya Chris ilitoka.

“Yes darling, za huko?”

“Nzuri tu mama. Unaendeleaje huko?”

“Nipo vizuri tu, nimekukumbuka mpenzi, hata usingizi umekata kabisa.”

“Kweli mpenzi?”

“Kweli kabisa.”

“Nataka kuuliza kitu dear maana naona dalili mbaya.”

“Dalili mbaya za vipi mpenzi?”

“Kuhusu mapenzi yetu.”

“Mh! Mbona sikuelewi? Hebu niulize.”

“Unanipenda kweli mama?”

“Nakupenda sana.”

“Unakumbuka nilikuambia nini kuhusu mzee wangu?”

“Nakumbuka.”

“Sasa hapo ndipo kwenye tatizo. Baba ameendelea kushikilia msimamo kuwa nioe mwanamke kutoka kijijini kwetu. Kuna kitu tunatakiwa kufanya mpenzi wangu ili tuweze kufanikisha jambo hili.”

“Mh! Kweli kuna kazi, kwa hiyo hutanioa Chris kwa sababu hiyo? Kumbuka mimi nakupenda na nimekuwa tayari kufanya kila kitu kwa ajili yako. Sipo tayari kukupoteza.”

“Najua, ndiyo maana nimekuambia, kuna jambo inabidi lifanyike ili tufanikishe.”

“Ni jambo gani mpenzi wangu?”

“Nimeshamwambia baba kuwa nimepata mchumba kijijini, sasa unachotakiwa kufanya.

Itabidi nikazungumze na baba mdogo kuhusu jambo hili ili wewe uende kijijini, ukakae kwa muda, mzee ajue unatokea kule. Lengo langu ili mambo yaweze kwenda bila matatizo, itawezekana kweli mpenzi wangu?” akasema Chris.

“Kwa nini ishindikane wakati nakupenda baba?”

“Sasa itakuwa lini?”

“Panga wewe. Wiki mbili zijazo tunamalizia muhula, tunafunga chuo kabla ya kurudi tena kumalizia chuo kabisa.”

“Safi kabisa, ngoja nijipange ndani ya muda huo mama. Vipi, nyumbani hakutakuwa na tatizo?”

“Hapana, nitajua cha kufanya. Niamini mimi.”

“Sawa mpenzi wangu, angalau sasa nina amani. Naweza kupata usingizi wangu vizuri nashukuru sana mama, usiku mwema.”

“Nawe pia.”

Mwanga wa ndoa yake na Laura ulionekana wazi kabisa. Moyo wake ukagubikwa na furaha ya ajabu. Haikuwa kazi ngumu tena kupata usingizi. Kilichobaki ilikuwa ni utekelezaji tu!



DK. Chris aliandika maneno fulani kwenye kadi alilokuwa nalo mkononi kisha akayarudisha tena macho yake kwa mgonjwa aliyekuwa ameketi mbele yake. Alikuwa mwanamke anayeelekea kuwa na umri si zaidi ya miaka 30. Alikuwa mpole, mkimya na anayeonekana kuhitaji huduma ya haraka sana. Hiyo ilikuwa ni muda mfupi baada ya kwenda maabara kutoa vipimo



. Aliitwa Sandra.



“Kuna tatizo kwenye mkojo wako. Una maambukizi. Kitaalamu tunaita Urinary Tract Infection, kwa kifupi UTI. Pia una malaria kali. Kwa namna hali yako ilivyo, ni lazima tukulaze ili tukuanzishie drip za kwinini mara moja ambayo inaweza kutibu malaria vizuri na haraka zaidi. Nitakupa na Antibiotics kali kwa ajili ya UTI.



“Hata hivyo lazima uwe makini sana matumizi ya vyoo, ambavyo hasa ndiyo chanzo kikuu cha maambuzi ya UTI. Pole sana Sandra,” alisema kwa sauti tulivu sana Dk. Chris.



“Ahsante dokta.”

“Ngoja nimuite sista aje kukuchukua,” akasema Dk. Chris.

Akainua mkonga wa simu iliyokuwa mezani kisha akabonyeza namba fulani na kuanza kuzungumza na upande wa pili. Muda mfupi baadaye alifika na kukabidhiwa kadi la Sandra, kisha akaongozana naye wodini. Mgonjwa mwingine akaingia.



Ndivyo siku ya Dk. Chris ilivyokuwa kazini kwake, Hospitali ya Kinondoni siku hiyo. Ilikuwa siku ambayo alidili na wagonjwa wa kawaida tu. Hakuwa na ratiba ya upasuaji siku hiyo.

***

Ilikuwa lazima apange safari ya Singida haraka iwezekavyo. Baba yake mzee Shila asingemwelewa hata kidogo kama angeendelea kuchelewa kuoa. Tayari alishatengeneza mazingira mazuri ofisini kwake.

Ni muda ambao hata Laura naye alikuwa ameshafunga chuo baada ya kumaliza mitihani. Ilikuwa ni kipindi cha likizo fupi ya wiki mbili. Hizo zilitosha kabisa kukamilisha mpango waliokubaliana.



Chris alisafiri hadi Singida ambapo alikutana na Laura na kuweka mipango yao sawa. Hakuwa na hofu tena, alishaamini kabisa kuwa Laura hakuwa mke wa mtu kama alivyojulishwa awali.

Hata hivyo kwa hofu ya usalama wake, hakuwa tayari kukutana naye katika hoteli ileile ya awali. Alifikia hoteli nyingine iliyokuwa nje kidogo ya mji.



“Laura unanipenda kweli? Kumbuka hapa nakwenda kufanya usaliti lakini ni kwa ajili ya penzi letu.”

“Najua baba, nakupenda, niamini.”

“Ahsante mama, sidhani kama tunatakiwa kutoka, maana kesho asubuhi tunakwenda kijijini. Mipango yote nitakuambia hukohuko, sawa mpenzi wangu?”



“Nimekuelewa baba.”

Walilala wakiwa na matumani makubwa ya kufanikisha mpango uliokuwa mbele yao; mpango wa ndoa. Safari haikuwa mbali sana.

Ni kesho tu!

***

Walishuka katika kituo cha Ibaga saa kumi jioni ikiwa ni safari ya takribani saa tano kutoka Singida Mjini hadi hapo katika mji mdogo wa Ibaga.

Kama miundombinu ingekuwa mizuri, ni safari ya saa mbili tu tena kwa mwendo wa kawaida. Walikuwa wachovu sana kwa safari hiyo. Walitafuta nyumba ya wageni na kulipia. Hapo ndipo filamu ilipotakiwa kuanza rasmi.



“Lazima mavazi yako yabadilike sasa, utavaa zile nilizokununulia mjini. Unapaswa kufanana na watu wa huku. Mchezo ulivyo ni kwamba, leo mimi nitakwenda nyumbani - Mkalama, wewe utalala hapa hadi kesho.

“Nitakwenda kuzungumza na baba mdogo ambaye anajua kila kitu kuhusu wewe, halafu yeye atazungumza na bibi kwamba, wewe utakuja kututembelea. Pale ndiyo sehemu ya kuchukua pointi, usilaze damu, ujitahidi kuendana na kila kitu cha pale nyumbani.



“Kwa bahati nzuri, hakuna shida sana, halafu kipindi hiki si cha kilimo kwa hiyo hawatakupeleka shamba. Kifupi uonyeshe heshima na mwonekano wa mtu wa kijijini usiyejua mambo ya mjini sana.

“Lakini itabidi tudanganye kuwa, hufahamu vizuri lugha yetu kwa sababu wazazi wako walihamia Mwanza tangu ukiwa mdogo lakini sasa wameamua kurudi tena kijijini. Mambo mengine utaniachia mimi.



Umenipata?” akasema Chris.

“Nimekuelewa vizuri sana.”

Mpango mzima ukawa umekamilika, ilibaki utekelezaji tu!

***

Chris alikodi baiskeli kutokea Ibaga hadi Mkalama, kijijini kwao. Alifika baada ya nusu saa tu. Alipokelewa vizuri na baba yake mdogo ambaye alimpa mpango mzima ulivyokuwa.

“Wazo zuri sana Chris, acha nizungumze na bibi. Naamini naye atafurahi. Hatajua mchezo wetu na inabidi iwe siri yetu tu,” akasema Shamakala.

“Sawa baba mdogo.”



“Zoezi linafanyika lini?”

“Hakuna kusubiri, ni kesho tu baba mdogo.”

“Sawa.”



CHRIS hakutaka kupoteza muda, kilichokuwa akilini mwake ni mke tu. Hakutaka mwanamke mwingine zaidi ya Laura. Baba yake mdogo, Shamakala alikubaliana na wazo lake.

Hakuwa na sababu ya kupoteza muda. Alimfuata mama yake, alipokuwa amekaa kisha akaketi kwenye kigoda jirani yake.



“Mkombi...” (Mama) Shamakala aliita kwa Kinyiramba.

“Shamakala unasemaje?”

“Kuna jambo zuri nataka kukuambia.”

“Zuri? Hebu nikae vizuri sasa. Haya niambie ni nini?”

“Ni kuhusu Chris... anataka kuoa.”



“Jambo zuri sana hilo. Ameshapata huyo mwali mwenyewe sasa?”

“Ndiyo, tena ni mtu wa hukuhuku kwetu.”

“Wa wapi?”



“Anatokea Kijiji cha Mpambala.”

“Safi sana, sasa mmefikia wapi?”

“Anataka kesho amlete hapa nyumbani aje kututembelea, kama tena taratibu zetu, tukikaa naye hapa japo kwa siku mbili tutaweza kumchunguza japo kidogo unavyojua na sisi ili tujiridhishe kuwa anafaa kuingia kwenye familia yetu.”

INAENDELEA
Powered by Blogger.