KARIBU USOME HADITHI NZURI ZA KUSISIMUA

SIMULIZI: Sitasahu sehemu ya Saba (7)


Pin by Larry Plummer on Eyes | Tears in eyes, Tears photography ...
Hakika niliongea na muhudumu na kunifanyia Booking ya chumba cha stahiki yangu. Baada ya yote hayo nikajiuliza ni usafiri gani ambao ningeutumia kwenda huko kati ya Ndege au Boat. Hapo nilikuwa na uamuzi wa haraka sana. Sikuwahi safiri na chombo chochote cha majini nikaona hii ni fursa ya kipekee kutimiza ndoto hizo. Usafiri wa Boti ukawa chaguo lisilo na upinzani.

Bila kuchelewa, asubuhi ya saa kumi na mbili nilikuwa barabarani naelekea bandarini kwa ajili ya safari hiyo. Kutokana na foleni kubwa ya Dar Es salaam nikajikuta nakosa usafiri wa saa moja. Hivyo nikapata usafiri wa saa tatu na nusu asubuhi. Ni baada ya kupata tiketi kutoka ofisi za Azam Merine zilizoko hapo hapo Bandarini.

Saa tatu na nusu tayari nimo ndani ya Boti ya Kilimanjaro nikielekea Zanzibari. Hakika ilikuwa safari nzuri sana kwangu ukizingatia ilikuwa mara yangu ya kwanza kutumia usafiri wa majini. Pia sikuweza kukaa ndani kutokana na hofu ya kutapika. Basi nikakaa juu kabisa ambako kuna hewa na upepo unapatikana kwa wingi. Upepo ambao ulinisaidia nisitapike.

Masaa mawili baadae nilikuwa nateremka bandarini Unguja, kila abiria alikuwa mwenye furaha kubwa ya kufika salama. Nje ya geti nikaiona gari yenye maandishi ya Hoteli ya Melia na pembeni yake kuna mwanaume ameshika bango lenye jina langu kuwa yeye ndiye atakayenipokea. Nikamuendea na kujitambulisha kwake huku nikitoa kitambulisho na kumkabidhi mtu yule. Haraka alichukua begi langu dogo na kuweka mlango wa nyuma ya gari lake kisha akanifungulia mlango wa mbele pembeni yake. Kitabia huwa sipendi kukaa mbele katika chombo cha moto labda mimi niwe ndie Dereva. Huwa navutiwa kukaa nyuma zaidi kwa imani kuwa inapotokea ajali ni nadra mtu wa nyuma kupata tatizo na hata akipata huwa bahati sana kufa. Imani niliyokuwa naishikilia kwa muda mrefu sasa.

Siku hiyo nilipenda kukaa pembeni ya dereva. Ni uamuzi huo uliokuja kunipa furaha kubwa maana niliweza kuyasawiri maeneo mengi ya Zanzibar. Huku nikistaajabu na hali ya ukimya niliokuwa naushuhudia barabarani. "Hakika Zanzibar ni mji wenye kuvutia sana" Nilijisemea. Wakati naendelea kuangalia mandhari ya mji wa Zanzibar nilikuja kushtukia tunafunguliwa Geti la Hoteli ya kisasa ya Melia. Kwa nje ilionekana hoteli nzuri sana kwa jinsi ilivyopambwa kwa namna ya kipekee kabisa. Jambo hilo likanifanya niwe na shauku ya kuingia ndani humo.

Ni baada ya dakika chache ya kufanya malipo, ndipo nilipokabidhiwa chumba cha kisasa kabisa ambacho kilinifanya niupongeze uamuzi wangu wa kuichagua Hoteli hii kwa ajili ya likizo yangu fupi. Nikajitoma Chumbani. Siku hiyo sikutoka nje ya Hoteli hiyo. Muda mwingi niliutumia kusoma na kutazama Tv. Siku zikasonga, muda ukatimia na majibu ya maswali yangu yakapata majibu.

Baada ya siku tatu tangu niwasili hapa Zanzibar na siku mbili nilizitumia kutembelea maeneo ya kihistoria. Nilianza kupapenda Zanzibari. Ilikuwa ni siku ya nne nyakati za asubuhi sana kama kawaida. Niliamka na kutoka nje ya Chumba changu kwa ajili ya kufanya mazoezi. Sikumbuki ilikuwa muda gani ila bado nakumbuka kila kitu. Ilikuwa kati ya saa moja asubuhi na saa mbili.

Nikiwa nimevalia mavazi ya kimazoezi baada ya kukimbia pembezoni mwa bahari na kuchoka sana. Ndipo nilipokuwa narejea taratibu kwa mwendo wa uchovu kutoka pwani ya Bahari mwa hoteli ya Melia.

Macho yangu yakanasa kiumbe kilichokuwa kimejilaza kwenye kiti cha uvivu ambacho wazee wengi wa maeneo ya Pwani hupenda sana kuvitumia viti hivyo...viti vya kulala ambavyo mara nyingi vinakuwepo maeneo ya beach zile kubwa na za gharama. Msisimko wa ajabu ukatawala mwili wangu ,nikajikuta nashikwa na bumbuwazi!.

Na kwa mara ya kwanza moyo wangu ukavutiwa na kiumbe kilicholala kama mita arobaini kutoka nilipo. Sijui kwa namna gani macho haya yaliweza kunasa kiumbe hicho. Ni wakati ambapo nikaanza kupoteza kujiamini kwangu. Nikajikuta hisia za uwoga zikianza kutambaa mwilini mwangu kama vile kitu fulani kibaya nimekiona. Nikajikuta moyo na macho yangu yakihitaji kuendelea kumtazama kiumbe huyo. Huku akili haikuweza kuhama kwenda sehemu nyingine kutokana na hofu ya kukipoteza kiumbe kinachoonekana mbeleni mwangu. Kila kiungo changu kikawa kinafanya kazi kwa namna ya ushirikiano wa ajabu. Kiumbe kikaonekana.

Hatua za miguu yangu zikaongezeka atimaye nikakaribia kumfikia kiumbe hicho. Hata hivyo sikuweza kufika mwisho kabisa ya lengo langu kabla ya kupigwa na butwaa. Nikasita. Mungu wangu! nikashtuka!. Ulikuwa mshtuko mkubwa sana kwangu. Hapo hapo nikajikuta sina namna nyingine niende mbele au nibadili mwelekeo wangu. Hata hivyo sauti ndani yangu ikaniambia " wewe ni mwanaume, na siku zote mwanaume husifiwa kwa ujasiri. 

Onesha uanaume wako" Nikatii sauti hiyo. Nikasogea na macho yakatua kwenye mwili wa binti mrembo. Akiwa amejilaza mahali hapo huku macho yake yakiwa yamefichwa na miwani mikubwa ya urembo ambayo siku hizi vijana wengi wanapenda kuyatumia. Bado nywele zake zikawa kama zinakaribia kugusa ardhi. Ardhi hisiyo na huruma, ardhi iliyomeza miili ya binadamu wengi. Ndipo nilipomtambua.

Nikamtambua kiumbe huyo na haraka nikaanza kurudisha kumbukumbu zangu nyuma. Ndio! Ni binti yule ambaye niliwahi kumgonga kule Posta. Duh! . Ni wakati huo huo binti nae akivua miwani yake na kubakia akinishangaa. Sikuwa nafahamu kwanini alikuwa ananishangaa? Nikaanza kujiuliza amenionaje mimi, ni kwamba sistahili kuwa hapa au ameshtushwa uwepo wangu mahali hapa?. Mwisho nikajiona mpuuzi kuwaza vitu ambavyo sikuwa na uhakika navyo. Nikajikuta namsalimia kiumbe huyo. Jibu lake lilikuwa tofauti na nilivyofikiria.

Nilifikiri hasingeweza kupokea salamu yangu. Alinijibu kwa upole na huku akinisindikiza na tabasamu zuri lililonifanya nibabaike kidogo. Niliomba kujumika nae mahali hapo kama hatajali. Jibu lake lilinishangaza pia, hakika hakuwa na hiana hata kidogo alinikaribisha kwa uchangamfu wa aina yake. Nilivuta kiti ambacho hakikuwa mbali na eneo hilo. Tukazungumza.

Tulizungumza mambo mengi sana. Ni wakati wa mazungumzo hayo ndipo nilipouona uzuri maradufu wa binti huyo ambaye alinikumbusha jina lake kuwa anaitwa Tayana, Tayana Masenga. Hakika siku zote nilitambua ya wazi ni msichana mrembo. Hata hivyo sasa ndio nagundua ni msichana mrembo zaidi kuliko nilivyofikiri, zaidi nilivyomuona mbali kwa mara ya kwanza. Ni mrembo hasa. Alikuwa msichana anayeonekana ana akili nyingi huku akiwa ni mwanamke mwenye kujiamini. Nikagundua pia ni mwanamke anayejua nini anachokifanya. Tukaendelea kuzungumza.

Ni katika mazungumzo hayo ndipo alipoonekana kushtushwa na mabadiliko makubwa niliyonayo. Kiukweli tangu niajiriwe nilibadilika sana. Hata mwili ulianza kujiachia. Huwezi kuniweka kwenye kundi la wanene na pia huwezi kuniweka kwenye kundi la watu wembamba. Nilikuwa mtu mwenye mwili wa wastani. Hakika hakutegemea kunikuta mahali hapo ila kwa kauli yake aliamini kuwa siku moja tutaonana. Nilimuuliza kwanini yupo pale? Alinijibu kuwa yupo pale kwa ajili ya likizo yake ambayo kampuni ilimpa kwa ajili ya kupunguza mawazo. Ni hapo ndipo nilijawa na udadisi wa kujua kipi kilimsibu mpaka apewe likizo ya kuondoa "stress'' Maana si kazi rahisi hata kidogo.

******************
ITAENDELEA


Powered by Blogger.