KARIBU USOME HADITHI NZURI ZA KUSISIMUA

Simulizi : Singidani Sehemu Ya Kumi na Nne (14)

Simulizi ya singidani
Usiku, Chris ndiye aliyempeleka mzee Ngeleja uwanja wa ndege kwa safari ya kurudi nyumbani kwake Mwanza. Ilikuwa furaha kubwa sana kwa Chris.

***

Ilikuwa kama ndoto lakini ndivyo ilivyokuwa. Chris alikuwa na Laura mbele ya Kanisa la KKKT, Azania Front akifunga ndoa na mwanamke aliyempenda kutoka moyoni mwake.



Kanisa lilikuwa limejaa, wazazi, ndugu, jamaa na wasanii wakubwa wa Bongo Movies kama Jaybee, Ramsey, Thaiyway na wengine wengi.



Mchungaji Massawe alianza kwa kumwuliza Chris: “Christopher Joseph Shila, upo tayari kuoana na huyu Laura John Ngeleja awe mke wako, ushirikiane naye katika shida na raha, hadi kifo kiwatenganishe? Kama ndivyo, sema ndiyo Mungu anisaidie.”

Chris hakujibu kitu!



HISIA kali ilimshika Chris. Ni kama alikuwa kwenye ndoto ya kusisimua. Hakuamini kama ni yeye alikuwa mbele ya kanisa akiwa amevaa suti kali nyeusi na shati jeupe huku shingoni akiwa amevaa tai fupi nyekundu!

Laura alitingisha! Alivaa gauni jeupe na shela iliyoburuzika hadi chini. Furaha ikamfanya asahau kuwa yupo kanisani na alitakiwa kujibu swali la Mchungaji ili kukamilisha uhalali wa ndoa yao.

Kanisa zima lilikuwa kimya. Wengine walianza kuogopa, wakahisi huenda Chris aliamua kubadilisha mawazo. Kwamba aliamua kuachana na suala la ndoa na Laura.

Haikuwa hivyo.

Chris alimpenda sana Laura, alichanganywa na tukio lililokuwa mbele yake ambalo lilikuwa kama sinema ya kusisimua.

“Christopher...” Mchungaji akaita.

“Naam!”

“Hujaona sehemu ya kusoma kijana wangu?” akauliza Mchungaji.

“Nimeona.”

“Sawa, nami nitakuuliza tena: “Christopher Joseph Shila, upo tayari kuoana na huyu Laura John Ngeleja awe mke wako, ushirikiane naye katika shida na raha, hadi kifo kiwatenganishe? Kama ndivyo, sema ndiyo Mungu anisaidie.”

“Ndiyo Mungu anisaidie,” akajibu Chris.

Ukumbi mzima ukalipuka kwa shangwe na nderemo. Matarumbeta nayo hayakuwa nyuma, yalisikika yakipulizwa na hivyo kuamsha shangwe ukumbini humo.

Mchungaji akamgeukia Laura kisha akamwuliza: “Laura John Ngeleja, upo tayari kuoana na huyu Christopher Joseph Shila awe mume wako, ushirikiane naye katika shida na raha, hadi kifo kiwatenganishe? Kama ndivyo, sema ndiyo Mungu anisaidie.”

“Ndiyo Mungu anisaidie,” akajibu Laura.

Kelele zikazidi kuwa kubwa, kanisa zima lilishangilia. Ilikuwa furaha kwa wote. Zoezi lililofuata baada ya hapo ilikuwa ni kuvalishana pete.

Ndoa ikawa imefungwa!

Chris na Laura wakawa mume na mke rasmi.

***CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Sherehe ilikuwa katika Ukumbi wa Mlimani City. Hiyo ilikuwa ni baada ya maharusi na ndugu wengine kuzunguka sehemu mbalimbali za jiji na kupiga picha.

Waandishi wa habari walikuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanapata picha nzuri za kupamba magazeti yao. Chris kuoa ilikuwa habari kubwa sana kwa magazeti Pendwa Bongo.

Waandishi na wapigapicha maarufu, Issa Mnally, Richard Bukos na Shakoor Jongo walikuwa wanashindana kutafuta picha bora zaidi ambayo ingependekezwa kutokea kwenye ukurasa wa mbele wa Gazeti la Ijumaa Wikienda siku ya Jumatatu.

Achana na hao, wapigapicha wa magazeti mengine ya kila siku na michezo walipigana vikumbo kupata picha nzuri. Msanii wa Bongo Muvi kuoa halikuwa jambo dogo!

Ndani ya Ukumbi wa Mlimani City, wasanii walikuwa wengi sana. Walialikwa watu maalum tu. Viongozi kadhaa wa kiserikali walikuwemo, wabunge, mawaziri, wakuu wa wilaya na madaktari.

Ilikuwa sherehe yenye heshima kubwa sana. Chris alijisikia mwanaume kamili kati ya wanaume. Wapambe wao walikuwa ni wasanii wa filamu, Jaybee na mkewe Vanessa.

MC wa shughuli hiyo alikuwa ni Chika, ambaye siku zote amekuwa akiongoza hafla mbalimbali za wasanii na watu wengine. Kwa Chris ilikuwa siku mpya ya kipekee ambayo ilikamilisha haja ya moyo wake.

Wenye kunywa walikunywa sana. Chakula kililiwa hadi kikabaki. Fungakazi ilikuwa zawadi, watu walitoa zawadi nyingi sana, achilia mbali wazazi wa pande zote ambao waliwazidi wote.

Alianza mzee Shila: “Umefanya kitu kikubwa sana mwanangu. Leo umenifanya nijisikie baba yako kamili. Nakupenda sana mwanangu. Kuhusu namna ya kuishi na mwenzako tumeshazungumza mengi, najua umeyashika.

“Kuna kitu ambacho nataka kukisema mbele ya watu wote hapa. Kwa tendo hili, nasema kwamba nimebadili fikra zangu. Nilichukia sana mwanangu kutokuoa mapema, lakini sikutaka kusikia anaoa mjini.

“Akilini mwangu niliamini wasanii wote ni wahuni, wana tabia mbaya na ni watu wasiofaa kwenye jamii. Kumbe nilikuwa nawaza tofauti. Nikadhani mke sahihi lazima atokee kijijini, kumbe siyo kweli.

“Leo hii mwanangu amepata mke mwema, sahihi na mzuri ambaye atamsaidia kama vitabu vinavyosema. Ninawabariki wanangu, mkaishi kwa amani na upendo. Kuanzia sasa, sina kinyongo na kazi ya mwanangu Chris. Pamoja na kwamba nilikulazimisha kusomea udaktari, nashukuru unaifanya kazi hiyo vizuri.

“Unasaidia kuokoa maisha ya Watanzania wengi kupitia taaluma yako. Wakati ukifanya yote hayo, bado pia unafanya sanaa kama sehemu ya kipato na fani uliyoichagua na kuipenda.

Kuhusu zawadi, najua una gari la kutembelea, lakini mimi nimekununulia jingine, litakalofanana na hadhi yako ya ubaba, maana sasa umekuwa baba. Nimekununulia Toyota Range Rover, iko hapo nje. Funguo zake hizi hapa,” akasema mzee Shila na kwenda kumkabidhi.

Shangwe zikaibuka upya!

Chris alipokea funguo za gari, kisha akanyanyua mkono juu na kuwaonyesha wageni ukumbini. Ghafla akagonganisha macho na mtu ambaye hakutarajia kabisa kumuona!

Chris alishtuka sana!



MSHTUKO ulikuwa mkubwa kwa hakika, kumuona mtu yule ambaye pia hakumwalika na alikuwa na uhakika kuwa Laura naye hakumwalika, kulimchanganya sana.

Akajitahidi kujikaza. Akaweka zile funguo za gari alizokabidhiwa na baba yake mfukoni. Baba yake akarudi kwenda kukaa sehemu yake. Chris alipomwangalia Laura akagundua kuwa, naye alikuwa amemuoana yule mtu.

Alikuwa ni Julius.

Jully, yule mwanafunzi aliyekuwa akisoma na Laura chuo Singida. Ni Jully ndiye aliyesaidia kuwaunganisha. Kwa maneno mengine kama si yeye, usiku ule pale club, kulikuwa na uwezekano mkubwa kwa Chris kumkosa kabisa Laura.

Zoezi la zawadi likaendelea ambapo Mzee Ngeleja alitangaza kutoa ekari 50 za mashamba ya mpunga, yaliyopo Mbarali, Mbeya. Ilipofika zamu ya wageni waalikwa, Jully naye alikwenda.

Alitoa bahasha ya kaki kwenye sehemu ya kuwekea zawadi kisha akamsogelea Chris na kumpatia karatasi ndogo.

“Hongera sana kaka, usijiulize ningekujaje hapa, ila naomba unitafute baada ya fungate, namba zangu zipo humu kwenye karatasi, kuna jambo lazima nikuambie.”

“Poa.”

Akatoka hapo na kwenda kwa Laura. Akamkumbatia na kumpongeza.

***

Tayari mipango yote ya fungate ilikuwa imefanyika. Wazazi wa bwana na bibi harusi waliamua kuchangia fedha kwa ajili ya safari ya watoto wao.

Ulikuwa muunganiko mzuri sana wa familia hizo mbili. Wazazi waliwataka watoto wao wachague kisiwa chochote duniani, waende wakastarehe kwa wiki mbili katika kufurahia ndoa yao mpya.

Kitu cha kushangaza ni kwamba, wote kwa pamoja walikubaliana kwenda Zanzibar. Wazazi walishangaa.

“Kwa nini Zanzibar?” Mzee Ngeleja aliuliza.

“Kwanza ni hapahapa Tanzania, tunapenda kufanya utalii wa ndani baba. Lakini pia tuna mambo mengi sana ya kufanya kama wanandoa, hatutaki kwenda mbali wala kutumia muda mrefu kwa ajili ya fungate.

“Wiki moja itatosha sana mjini Zanzibar kwa mapumziko ya fungate yetu, wiki nyingine tutakwenda Singida, halafu tutarudi Dar kuendelea na mambo mengine.”

Hakuna aliyepinga, Mzee Ngeleja na Mzee Shila wakakubaliana kwa pamoja na watoto wao. Walilala The Atriums Hotel iliyopo Sinza–Afrika Sana ambapo asubuhi ya saa 4:00 waliondoka hadi uwanja wa ndege walipopanda ndege na kuelekea visiwani Zanzibar.

***

Wakiwa wamejipumzisha kwenye bustani ndani ya Hoteli ya Karafuu mjini Unguja wakicheza michezo ya kimapenzi, Chris akamkumbuka Jully.

“Mh! Lakini Jully anaonekana ana jambo muhimu la kuniambia, lakini sijajua ni nini. Ngoja nikachukue ile namba yake ya simu ndani,” akasema Chris.

“Hapana dear, ngoja nikachukue. Umeweka wapi?”

Chris akamwelekeza.

INAENDELEA

Powered by Blogger.